Mtu anayezungumza lugha mbili dhidi ya mkalimani: Je, tofauti ni nini?
Wakalimani wote wana lugha mbili, lakini si watu wote wanaozungumza lugha mbili wanaweza kuwa wakalimani.
- Mkalimani ni mtaalamu aliyefunzwa lugha mbili mwenye ujuzi wa tamaduni mbili ambaye amefungwa na kanuni za maadili. Kiwango cha jamii cha kufanya kazi kama mkalimani nchini Australia ni kuthibitishwa na NAATI.
- Mtu anayezungumza lugha mbili anaweza kuzungumza lugha mbili lakini hajapata mafunzo kama mkalimani na hafungwi na kanuni za maadili.
Je, ni nini kinachofanya wakalimani kuwa tofauti?
Mafunzo na Uthibitisho
Wakalimani wanahitaji mafunzo rasmi ili kukuza ujuzi unaohitajika kufanya kazi kitaaluma. NAATI huangalia ujuzi na uzoefu wao kabla ya kutoa cheti, ili uweze kuwa na uhakika kwamba uwezo wao umetathminiwa.
Ujuzi wa lugha na uhamisho
NAATI hutathmini ujuzi mbalimbali ili kuhakikisha wakalimani wako sahihi na wenye utaalum. Hii inajumuisha uwezo wa lugha, kumbukumbu, kujiamini katika kuomba ufafanuzi, usimamizi wa usemi unaoingiliana, uwezo wa kuendana na sauti na mtindo wa wazungumzaji, n.k. Wakalimani wana ujuzi wa kutambua maana za kitamaduni katika kile kinachosemwa na kuziwasilisha vizuri katika lugha nyingine.
Mwenendo wa kitaaluma
Wakalimani hufuata kanuni za maadili zenye kanuni tisa zinazowaongoza. Kwa mfano, wakalimani lazima wawe sahihi, wasioegemea upande wowote na wa siri. Hawatashiriki taarifa bila kibali (isipokuwa inapohitajika na sheria). Pia wana ujuzi wa kusimamia matatizo ya kimaadili katika kazi zao.
Maarifa maalum
Wakalimani wengi huzingatia nyanja maalum kama vile sheria au huduma ya afya. Hii huongeza uwezo wao wa kutafsiri kwa usahihi wanapojenga ujuzi wa istilahi na hali. NAATI hutoa sifa za Mkalimani Mtaalamu Aliyeidhinishwa katika baadhi ya lugha kwa wakalimani ambao wamebobea sana katika mazingira ya afya au kisheria.
Watu wanaozungumza lugha mbili wanaotumika kama wakalimani
Kukosa ujuzi
Mtu anayezungumza lugha mbili anaweza kuwa fasaha katika lugha mbili lakini hana ujuzi wa kuhamisha maana kati yao. Huenda wakakosa kujiamini katika kuomba ufafanuzi au uzoefu wa kuandika madokezo, ambao ni ujuzi muhimu wakati kuna taarifa changamano. Huenda wakakosa msamiati kwa hali rasmi au ngumu.
Hatari ya kutowasiliana vizuri
Kuwaomba watu wanaosema lugha mbili wasiofunzwa kutafsiri katika hali za kisheria, kimatibabu au nyingine nyeti kunaweza kusababisha makosa makubwa. Hizi zinaweza kusababisha utambuzi mbaya, kutoelewana kwa haki za kisheria, masuala ya kibali au uvunjaji wa usiri.
Haijapimwa
Ujuzi wao wa lugha na ukalimani haujatathminiwa na mtu anayejitegemea.
Wanafamilia kuwa wakalimani
Kutumia wanafamilia kama wakalimani husababisha matatizo ya ziada:
- Wanaweza kufanya makosa hatari kutokana na ukosefu wa istilahi au kwa kuongeza au kuondoa taarifa kwa sababu za kihisia, kitamaduni au kibinafsi
- Wanaweza kusimulia toleo lao lenyewe la matukio
- Watu wanaohusika wanaweza wasishiriki taarifa zote muhimu kwa sababu za faragha
- Inaweza kusababisha msongo wa mawazo na kiwewe kwa mwanafamilia
Hakuna mtu aliye chini ya umri wa miaka 18 anayepaswa kuombwa kutafsiri. Kumtuma mkalimani mtaalamu huwezesha familia kuzingatia kutoa msaada wa kihisia na kuuliza maswali.
Ambapo watu wanaozungumza lugha mbili hufanikiwa
Wakati mawasiliano ni kama hatari ndogo na usahihi si muhimu, watu wanaozungumza lugha mbili huchukua jukumu muhimu. Wafanyakazi wanaozungumza lugha mbili hutumika kama wapokeaji, wauguzi, maafisa wa utawala, wataalamu wa uuzaji, waongoza watalii na zaidi. Uwezo wao wa kuzungumza lugha mbili huboresha mawasiliano ya jamii.
Katika huduma ya afya, wafanyakazi wa afya wanaozungumza lugha mbili wanao asili ile ile ya kitamaduni ya mgonjwa huchukua jukumu muhimu katika kutoa huduma inayofaa kitamaduni. Hata hivyo, kila mara tumia mkalimani wakati:
- kibali kinapotolewa
- utambuzi, mipango ya matibabu na hali zingine muhimu au za kihisia zinapojadiliwa.
Maswali ya kuuliza
Unapochagua kati ya mkalimani na mtu anayezungumza lugha mbili, fikiria:
- Je, kuna athari za kimaadili?
- Je, kutoelewana kunaweza kuwa na matokeo mabaya makubwa?
- Je, mazungumzo au taarifa hiyo inamfunga mtu kisheria?
- Je, ninahitaji kutoa au kupokea kibali?